Mudavadi awataka Wakenya kuzingatia sheria ili kudumisha amani

Jul 26, 2024 - 17:40
 0
Mudavadi awataka Wakenya kuzingatia sheria ili kudumisha  amani
Waziri Mkuu katika Wizara Musalia Mudavadi. Picha/hisani.

Na Robert Mutasi 

Waziri Mkuu  katika Wizara Musalia Mudavadi amewataka Wakenya kutii sheria hata wanapohisi kukerwa na mwelekeo ambao serikali inachukua.

Huku akikiri kuwa Kenya inakabiliwa na wakati mgumu, Mudavadi alisisitiza kuwa hali ya taifa hilo haipaswi kutumiwa kisingizio cha kueneza ukosefu wa utulivu.

“Tuwe wazalendo. Hata tunapokuwa na matatizo lazima tuhakikishe tunafuata sheria tunapotaka kusikilizwa,” alisema.

Mudavadi alisema hayo Ijumaa, Julai 26, 2024, wakati wa mazishi ya Susan Wanjohi, mamake Katibu wa Baraza la Mawaziri Mercy Wanjau huko Nanyuki, Kaunti ya Laikipia.

Soipan Tuya, Alice Wahome, Rebecca Miano, na aliyekuwa Katibu wa Baraza la Mawaziri la Hazina ya Kitaifa Njuguna Ndung'u walikuwa miongoni mwa walioteuliwa katika baraza la mawaziri waliohudhuria, pamoja na Naibu Rais Rigathi Gachagua.

Mudavadi alielezea masikitiko yake kwa idadi kubwa ya vifo na uharibifu wa mali uliosababishwa na maandamano ya hivi majuzi dhidi ya serikali.

Aliongeza kuwa itachukua muda kwa baadhi ya wafanyabiashara kupata nafuu kutokana na hasara waliyoipata.

"Watu wengi wamepoteza maisha yao. Wengine walikuwa na mikopo wanaihudumia. Wengine wamepoteza akiba yao ya maisha. Tunajua makampuni ya bima hayawalipi watu fidia wanapopoteza mali zao katika mazingira kama hayo," aliongeza.

Alidai kuwa sekta kadhaa za kiuchumi za kitaifa zimeathirika kutokana na maandamano hayo.

"Chochote tunachofanya, hatupaswi kusababisha matatizo kwa wale ambao hawana uhusiano wowote na kinachoendelea," alihimiza.

"Tumefanya makosa, sio mtindo kuwa na nchi kwenye shida," Mudavadi alikiri.

Mudavadi aliwataka vijana kufikiria kwa makini matatizo yanayokumba nchi hivi sasa. 

What's Your Reaction?

like

dislike

love

funny

angry

sad

wow