Wakenya kunufaika na afya bora kupitia Mswada wa Ubora wa Huduma

Jul 22, 2024 - 12:31
Jul 22, 2024 - 12:35
 0
Wakenya kunufaika na afya bora kupitia Mswada wa Ubora wa Huduma
Jumba la Wizara ya Afya. Picha/hisani.

Na Robert Mutasi 

Wakenya huenda wakanufaika na viwango bora vya matibabu iwapo Wizara ya Afya itakamilisha mswada wa Viwango vya Ubora wa Huduma na hatimaye kuupitisha kuwa sheria.

 Mswada wa Ubora wa Huduma unatarajiwa kujaza pengo kubwa katika huduma ya afya na kuimarisha uboreshaji wa afya kama utaratibu wa shirika kote katika hospitali za umma na za kibinafsi kulingana na azma ya kufikia vifo sifuri vya wagonjwa vinavyoweza kuzuilika.

Akizungumza wakati wa hotuba rasmi katika Kongamano la Uongozi la African Consortium for Quality Improvement Research in Frontline Healthcare (ACQUIRE) jijini Nairobi Jumatatu, Dkt. Kigen Bartilol, Mkurugenzi wa Viwango vya Afya, Kanuni za Uhakikisho wa Ubora katika Idara ya Serikali ya Afya ya Umma na Viwango vya Kitaalamu katika Wizara ya Afya, alitangaza kuwa sheria hiyo mpya itahakikisha kuwa vituo vya afya vya umma na vya kibinafsi kote nchini vinazingatia viwango vya utoaji huduma vilivyoidhinishwa.

"Itawawezesha wahudumu wa afya kutoa tathmini za punjepunje kwa vituo vya afya vinavyohusu miundombinu, uwezo wa rasilimali, watu na taratibu. Inapofanyika kwa usahihi na kwa kila mtu katika taasisi, tunatarajia wagonjwa kupata huduma bora za afya nchini kote,” alifafanua na kuongeza kuwa itaanzisha taasisi huru itakayosimamia na kuishauri serikali kuhusu masuala ya usalama na ubora katika huduma za afya, hivyo kuwa na uhakika wa kimataifa. 

Dkt. Kigen alisema kuwa Kenya inakabiliwa na mzigo mkubwa wa magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza na imefikia hatua ambapo mabadiliko katika uboreshaji wa afya ni muhimu kwa kufikia azma ya nchi ya Kushughulikia Afya kwa Wote.

Afya kwa Wote imeundwa kuyaziba mapengo katika Mfumo wa sasa wa Uidhinishaji wa Ubora wa Huduma wa Kenya ambao hauna miundo ya sharti la tathmini huru, inayowajibika na inayoaminika ya usalama na ubora wa huduma ya afya.

Mswada huo mpya unalenga vifaa vya hospitali kuweka utaratibu wa kufanya mabadiliko ya uboreshaji na utamaduni ili kuwezesha kujitathmini na kuzingatia tathmini za wenzao na wakaguzi wa nje ikiwemo bima za afya, idara za afya za kaunti, Wizara ya Afya, wadhibiti na mashirika ya uthibitishaji.

Akirejelea maoni yake, Dk. Lydia Okutoyi, Mkurugenzi wa Ubora wa Huduma za Afya katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta na mwanzilishi mwenza wa Muungano wa Afrika wa Utafiti wa Uboreshaji Ubora katika Huduma ya Afya ya Mstari wa mbele (ACQUIRE) alidokeza kuwa kusawazisha mbinu bora za utunzaji wa wagonjwa ni muhimu ili kuimarisha mifumo ya afya nchini Kenya itakayowezesha kupunguza vifo vinavyoweza kuzuilika.

"Mfumo wetu wa afya uko katika shida, unakabiliwa na changamoto kubwa kutoka kwa uhaba wa wafanyikazi na dawa hadi operesheni zisizoratibiwa za hospitali, ukosefu wa utayari wa kutosha kushughulikia magonjwa ya milipuko pamoja na mawazo ambayo yanazingatia matibabu ya magonjwa badala ya mwitikio wa mfumo mzima kwa wagonjwa. Hii inachangiwa na kuongezeka kwa gharama za matunzo, ukosefu wa vifaa vya kutosha, vinavyofaa, uhaba wa wafanyikazi, vikwazo vya udhibiti, na dawa ghali,” alisema.

Dk. Okutoyi alisema kuwa wahudumu wa afya chini ya mwavuli wa ACQUIRE wanaamini sheria mpya ya Ubora wa Huduma itainua viwango vya huduma za afya nchini kote kwa kuelekeza rasilimali, kujitolea, uwekezaji na kuendelea kwa wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na serikali, wasimamizi wa vituo vya afya, bima na matabibu.

Alitaja hitaji la dharura la uzoefu unaomhusu mgonjwa kama vile usajili sahihi, muda mfupi wa kupanga foleni, kuhifadhi na kurejesha rekodi za wagonjwa, maoni ya kila siku ya madaktari na wasimamizi, ziara za kufuatilia miongoni mwa mwengine mengi, akikubali kwamba uthibitisho wa kisheria utaungwa mkono na mfumo.

Aliweka wazi kuwa lengo la mfumo huo mpya ni kuimarusha utendakazi bora wa kibinadamu kwa kupunguza makosa, kuimarisha ubora wa huduma na malengo yanayomlenga mgonjwa. 

Dkt Okutoyi aliongezea kuwa ni wakati mwafaka sasa wa kuzibadilisha tabia na mienendo ya kitamaduni na kuukumbatia ubora, data kutoka kwa masiliano na ushirikiano mzuri ndani na katika taaluma zote za afya. 

What's Your Reaction?

like

dislike

love

funny

angry

sad

wow