Waziri Mteule Eric Muuga aahidi kulinda nyenzo jadilifu

Aug 2, 2024 - 16:10
Aug 2, 2024 - 20:00
 0
Waziri Mteule  Eric Muuga aahidi kulinda nyenzo jadilifu
Waziri Maji na Unyunyuziaji Eric Muuga. Picha/hisani.

Na Robert Mutasi 

Waziri mteule wa Maji na Unyunyuziaji Eric Muuga amefichua mbinu na mikakati atakayoweka kulinda nyenzo jadilifu kuhakikisha Wakenya wanapata maji ya kutosha.

Akifika mbele ya Kamati ya Bunge la Kitaifa kwa kuasisiwa mnamo Ijumaa, Agosti 2, 2024, Muuga amesema kuwa kulinda nyenzo jadilifu kutatua suala la uhaba wa maji.

Amesema kuwa atazindua kampeni ya kuhamasisha Wakenya kuwa na jukumu la kibinafsi la kulinda nyenzo za maji. 

"Tutawahamasisha Wakenya kwamba ni jukumu la kila Mkenya kuhifadhi kidogo alichonacho," alisema.

"Uhifadhi ni muhimu kwa rasilimali zinazoweza kurejeshwa," aliongeza.

Vile vile Waziri huyo amesisitiza kuwa atashughulikia suala la uharibifu wa nyenzo hizo na kuchukulia sheria wahusika. 

Amesema kuwa atadhibiti matumizi ya maji ili kuzuia kampuni na wananchi kukadiria hasara. 

"Neno langu kwa Wakenya ni kwamba, nitafanya kila niwezalo, nitatathmini zaidi kwa maji ambayo yanahesabiwa, maji ambayo yameunganishwa lakini hayamfikii mtumiaji," alisema.

Kwenye suala la usambazaji wa maji, ameahidi kuwa atahakikisha usambazaji asilimia mia wa maji ya mambo kwa watumizi katika maeneo tofauti nchini.

Ameahidi kuziba mapengo yote ambayo wananchi hutumia kutumia maji ya mabomba kwa njia za mkato. 

Ameapa kuongeza kipato katika Wizara ya Maji kwa kuhakikisha maji yanatumika ifaavyo. 

Kulingana na Muuga, Wizara ina maono ya kuhakikisha uunganishaji wa maji ya mabomba asilimia 100 ifikiapo mnamo mwaka wa 2030.

"Wizara ina maono ya kuhakikisha kwamba Wakenya wote wanaunganishwa kwa asilimia 100 kufikia 2030. Hii inakubaliana na Ajenda ya Maji ya Afrika 2063," alisema. 

Kulingana na Waziri huyo, asilimia 45 ya maji hayaongezei mapato katika uchumi wa taifa. 

"Nchini Kenya asilimia hiyo inaanzia takriban 45, yaani, maji ambayo hayana athari za kiuchumi moja kwa moja kwa watoa huduma za maji na pia kwa Wakenya," Muuga alisema

What's Your Reaction?

like

dislike

love

funny

angry

sad

wow